< Luka 6 >

1 Sasa ilitokea kwenye Sabato kwamba Yesu alikuwa akipita katika ya shamba la nafaka na wanafunzi wake walikuwa wakichuma masuke, wakayasuguasugua kati ya mikono yao wakala nafaka. 2 Lakini baadhi ya Mafarisayo wakasema, “Kwa nini mnafanya kitu ambacho si halali kisheria kukifanya siku ya sabato”? 3 Yesu, akawajibu, akisema, “Hamkuwahi kusoma kile Daudi alifanya alipokuwa na njaa, yeye na wanaume waliokuwa pamoja naye? 4 Alikwenda katika nyumba ya Mungu, na akachukuwa mikate mitakatifu na kuila baadhi, na kuitoa baadhi kwa watu aliokuwa nao kuila, hatakama ilikuwa halali kwa makuhani kuila.” 5 Kisha akawaambia, “Mwana wa Adamu ni Bwana wa Sabato.” 6 Ilitokea katika Sabato nyingine kwamba alikwenda ndani ya sinagogi na kuwafundisha watu huko. Palikuwa na mtu ambaye mkono wake wa kulia ulikuwa umepooza. 7 Waandishi na Mafarisayo walikuwa wanamwangalia kwa makini kuona kama angemponya mtu siku ya Sabato, ili waweze kupata sababu ya kumshtaki kwa kufanya kosa. 8 Lakini alijua nini walikuwa wanafikiri na akasema kwa mtu aliyekuwa amepooza mkono, “Amka, simama hapa katikati ya kila mmoja.” Hivyo huyo mtu akanyanyuka na kusimama pale. 9 Yesu akasema kwao, “Nawauliza ninyi, ni halali siku ya Sabato kufanya mema au kufanya madhara, kuokoa maisha au kuyaharibu?” Kisha aliwaangalia wote na kumwambia yule mtu, 10 “Nyoosha mkono wako.” Akafanya hivyo, na mkono wake ulikuwa umeponywa. 11 Lakini walijawa na hasira, wakaongeleshana wao kwa wao kuhusu nini wanapaswa wafanye kwa Yesu. 12 Ilitokea siku hizo kwamba alikwenda mlimani kuomba. Aliendelea usiku mzima kumuomba Mungu. 13 Ilipokuwa asubuhi, aliwaita wanafunzi wake kwake, na akawachagua kumi na wawili kati yao, ambao pia aliwaita “mitume.” 14 Majina ya wale mitume yalikuwa Simoni (ambaye pia alimwita Petro) na Andrea ndugu yake, Yakobo, Yohana, Filipo, Bartolomayo, 15 Mathayo, Tomaso na Yakobo mwana wa Alfayo, Simoni, ambaye aliitwa Zelote, 16 Yuda mwana Yakobo na Yuda Iskariote, ambaye alikuwa msaliti msaliti. 17 Kisha Yesu alitelemka pamoja nao toka mlimani na kusimama mahali tambarare. Idadi kubwa ya wanafunzi wake walikuwa huko, pamoja na idadi kubwa ya watu kutoka Uyahudi na Yerusalemu, na kutoka pwani ya Tiro na Sidoni. 18 Walikuja kumsikiliza na kuponywa magonjwa yao. Watu waliokuwa wakisumbuliwa na pepo wachafu waliponywa pia. 19 Kila mmoja kwenye hilo kusanyiko alijaribu kumgusa kwa sababu nguvu za uponyaji zilikuwa zikitokea ndani yake, na aliwaponya wote. 20 Kisha akawaangalia wanafunzi wake, na kusema, “Mmebarikiwa ninyi mlio maskini, kwa maana ufalme wa Mungu ni wenu. 21 Mmebarikiwa ninyi mlio na njaa sasa, kwa maana mtashibishwa. Mmebarikiwa ninyi mliao sasa, kwa maana mtacheka. 22 Mmebarikiwa ninyi ambao watu watakapowachukia na kuwatenga na kuwashutumu ninyi kwamba ni waovu, kwa ajili ya Mwana Adamu. 23 Furahini katika siku hiyo na kurukaruka kwa furaha, kwa sababu hakika mtakuwa na thawabu kubwa mbinguni, kwa maana baba zao waliwatendea vivyohivyo manabii. 24 Lakini ole wenu mlio matajiri! Kwa maana mmekwisha pata faraja yenu. 25 Ole wenu mlio shiba sasa! Kwa maana mtaona njaa baadaye. Ole wenu mnaocheka sasa! Kwa maana mtaomboleza na kulia baadaye. 26 Ole wenu, mtakaposifiwa na watu wote! Kwa maana baba zao waliwatendea manabii wa uongo vivyohivyo. 27 Lakini nasema kwenu ninyi mnaonisikiliza, wapendeni adui zenu na kufanya mema kwa wanao wachukieni. 28 Wabarikini wale wanao walaani ninyi na waombeeni wale wanaowaonea. 29 Kwake yeye akupigaye shavu moja, mgeuzie na la pili. Kama mtu akikunyang'anya joho lako usimzuilie na kanzu. 30 Mpe kila akuombaye. Kama mtu akikunyang'anya kitu ambacho ni mali yako, usimuombe akurudishie. 31 Kama mpendavyo watu wawatendee, nanyi watendeeni vivyo hivyo. 32 Kama mkiwapenda watu wawapendao ninyi tu, hiyo ni thawabu gani kwenu? Kwamaana hata wenye dhambi huwapenda wale wawapendao. 33 Kama mkiwatendea mema wale wanaowatendea ninyi mema, hiyo ni thawabu gani kwenu? Kwa maana hata wenye dhambi hufanya vivyo hivyo. 34 Kama mkikopesha vitu kwa watu ambao mnategemea watawarudishia, hiyo ni thawabu gani kwenu? Hata wenye dhambi huwakopesha wenye dhambi, na hutegemea kupokea kiasi hicho hicho tena. 35 Lakini wapendeni adui zenu na watendeeni mema. Wakopesheni na msihofu kuhusu kurudishiwa, na thawabu yenu itakuwa kubwa. Mtakuwa wana wa Aliye Juu, kwasababu yeye mwenyewe ni mwema kwa watu wasio na shukurani na waovu. 36 Iweni na huruma, kama Baba yenu alivyo na huruma. 37 Msihukumu, nanyi hamta hukumiwa. Msilaani, nanyi hamtalaaniwa. Sameheni wengine, nanyi mtasamehewa. 38 Wapeni wengine, nanyi mtapewa. Kiasi cha ukarimu - kilichoshindiliwa, kusukwasukwa na kumwagika - kitamwagika magotini penu. Kwa sababu kwa kipimo chochote mnachotumia kupimia, kipimo hicho hicho kitatumika kuwapimia ninyi.” 39 Kisha akawaambia mfano pia. “Je mtu aliye kipofu aweza kumwongoza mtu mwingine kipofu? Kama alifanya hivyo, basi wote wangalitumbukia shimoni, je wasingetumbukia? 40 Mwanafunzi hawi mkubwa kuliko mwalimu wake, lakini kila mtu akiisha kufundishwa kwa ukamilifu atakuwa kama mwalimu wake. 41 Na kwa nini basi wakitazama kibanzi kilicho ndani ya jicho la ndugu yako, na boriti lililo ndani ya jicho lako huliangalii? 42 Utawezaje kumwambia ndugu yako, 'Ndugu, naomba nikitoe kibanzi kilicho ndani ya jicho lako,' nawe huangalii boriti iliyo katika jicho lako mwenyewe? Mnafiki wewe! Kwanza itoe boriti katika jicho lako mwenyewe, ndipo utaona vizuri kutoa kibanzi katika jicho la ndugu yako. 43 Kwa sababu hakuna mti mzuri uzaao matunda mabaya, wala hakuna mti mbaya uzaao matunda mazuri. 44 Kwa sababu kila mti hutambulika kwa matunda yake. Kwa sababu watu hawachumi tini kutoka kwenye miba, wala hawachumi zabibu kutoka kwenye michongoma. 45 Mtu mwema katika hazina njema ya moyo wake hutoa yaliyo mema, na mtu mwovu katika hazina mbovu ya moyo wake hutoa yaliyo maovu. Kwa sababu kinywa chake husema yale yaujazayo moyo wake. 46 Kwanini mnaniita, 'Bwana, Bwana', na bado hamyatendi yale nisemayo? 47 Kila mtu ajaye kwangu na kuyasikia maneno yangu na kuyatendea kazi, nitawaonyesha jinsi alivyo. 48 Anafanana na mtu ajengae nyumba yake, ambaye huchimba chini sana, na kujenga msingi wa nyumba juu ya mwamba imara. Mafuriko yalipokuja, maporomoko ya maji yaliipiga nyumba, lakini hayakuweza kuitikisa, kwa sababu ilikuwa imejengwa vizuri. 49 Lakini yeyote asikiaye neno langu na hakulitii; mfano wake ni mtu aliyejenga nyumba juu ya ardhi pasipokuwa na msingi, mto ulipoishukia kwa nguvu, nyumba ile ilitopata maangamizi makubwa.

< Luka 6 >