< Yeremia 48 >

1 Juu ya Moabu, Yahwe wa majeshi, Mungu wa Israeli, asema hivi, “Ole kwa Nebo, kwani umekuwa ukiwa. Kiriathaimu umetekwa na kuaibishwa. Ngome zake zimeangushwa na kuaibishwa. 2 Heshima ya Moabu haipo tena. Adui zake katika Heshboni walipanga njama za kumwangamiza. Walisema, 'Njoni tumwangamize kama taifa. Madmena pia itaangamizwa - upanga utakutangulia.' 3 Sikilizeni! Sauti ya mvumo inakuja kutoka Horonaimu. 4 Moabu ameangamizwa. Vilio vya watoto wake vinasikika. 5 Wanapanda kilima cha Luhithi wakilia, njia yote kuelekea Horonaimu, vilio vinasikika kutokana na maangamizi. 6 Kimbieni! okeeni maisha yenu kama kichaka cha mreteni katika nyika. 7 Maana kwa sababu ya tumaini lenu katika matendo na utajiri wenu, ninyi pia mtatekwa. Kisha Kemoshi atachukuliwa matekani, pamoja na makuhani na viongozi wake. 8 Maana mwaribu atafika kila mji; hakuna mji utakaookoka. Hivyo bonde litaangamia na tambarare itateketezwa, kama alivyosema Yahwe. 9 Mpeni Moabu mabawa, maana ni lazima aruke mbali bila shaka. Miji yake itakuwa magofu, pasipo na mtu wa kuishi humo. 10 Na alaaniwe kila aliye mvivu katika kufanya kazi ya Yahwe! Na alaaniwe kila auzuiaye upanga wake usimwage damu! 11 Moabu amekuwa akijisikia salama tangu alipokuwa kijana. Yeye ni kama mvinyo wake ambao haujamiminwa kutoka mtungi kwenda mtungi mwingine. Hajaenda matekani. Hivyo radha yake ni njema kama mwanzo; radha yake haibadiliki. 12 Hivyo tazama, siku zinakuja - asema Yahwe - nitakapompelekea watakao mchovya na kumwaga mitungi yake yote na kupasua mitungi yake. 13 Kisha Moabu atamwaibikia Kemoshi kama ambavyo nyumba ya Israeli ilivyoiabikia Betheli, tumaini lao. 14 Utawezaje kusema, 'Tu askari, wapiganaji wenye nguvu'? 15 Moabu itaangamizwa na miji yake kushambuliwa. Kwa maana vijana wake wazuri wameshuka katika eneo la machinjo. Hili ni tamko la mfalme! Yahwe wa majeshi ndilo jina lake. 16 Maangazizo ya Moabu yanakaribia; maafa yanaharakisha. 17 Ninyi nyote mlio karibu na Moabu, ombolezeni. Nanyi mjuao fahari yake, pigeni kelele hivi, 'Ole, fimbo yenye nguvu, fimbo yenye heshima, imevunjwa.' 18 Shukeni kutoka mahali penu pa heshima na kuketi katika nchi kavu, ewe binti uishie Diboni. Maana aiangamizaye Moabu anakushambulia, atakayeziharibu ngome zako. 19 Simameni njiani na kuangalia, enyi mwishio katika Aroeri. Waulizeni wanaokimbia na kutoroka. Sema, 'Nini kimetokea?' 20 Moabu ameaibika, maana amevujwa. Lieni kwa sauti na uchungu; pigeni yowe kuomba msaada. Wambieni watu waliokando ya Mto Arinoni kwamba Moabu ameangamizwa. 21 Basi maangamizi yamefika katika nchi ya kilima, huko Holoni, Yakza, na Mefathi, 22 huko Diboni, Nebo, na Bethi Diblathaimu, 23 huko Kiriatahaimu, Beth Gamul, na Bethi Meoni, 24 huko Keriothi na Bozra, na katika miji yote iliyomo katika nchi ya Moabu - miji iliyoko mbali na karibu. 25 Nguvu za Moabu zimekwisha; mkono wake umevunjwa - asema Yahwe. 26 Mnywesheni, maana alitenda kwa kiburi kinyume changu, Yahwe. Basi Moabu anapiga makofi kwa machukizo kwa matapiko yake mwenyewe, hivyo amekuwa pia kitu cha kuchekesha. 27 Maana Israeli hakuwa kitu cha kuchekesha kwako? Alionekana miongoni mwa wezi, kwamba ulitikisa kichwa chako kwake mara ulipoongea juu yake? 28 Jitengeni na miji na kuweka kambi katika minuko, enyi watu wa Moabu. Kuwa kama njiwa anayeatamia juu ya mlango wa tundu katika miamba. 29 Tumesikia juu ya kiburi cha Moabu - majivuno yake, maringo, kiburi, utukufu binafsi na kujiinua moyoni. 30 Hili ni tamko la Yahwe - mimi mwenyewe najua maneno yake ya ukaidi, yasiyosaidia chochote, kama matendo yake. 31 Hivyo nitavumisha maombolezo kwa ajili ya Moabu, na nitapiga kelele katika uzuni kwa ajili ya Moabu. Nitaomboleza kwa ajili ya watu wa Kir Hereshi. 32 Nitalia zaidi kwa ajili yenu kuliko nilivyofanya kwa Yazeri, mzabibu wa Sibma! Matawi yako yalipita katika Bahari ya Chumvi na kufika hata Yazeri. Mwaribu ameshambulia matunda yenu ya kiangazi na mzabibu wenu. 33 Hivyo sherehe na furaha vimeondolewa kutoka miti ya matunda na nchi ya Moabu. Nimekomesha mvinyo kutoka mashinikizo yao. Hawatakanyaga kwa kelele za furaha. Kelele yoyote haitakuwa kelele ya furaha. 34 Kutoka kelele huko Heshiboni hata kufika Eleale, sauti yao inasikika hata Yahazi, kutoka Soari hata Horonaimu na Eglathi Shelishiya, hata maji ya Nimrimu yamekauka. 35 Maana nitamkomesha kila mtu katika Moabu atoaye sadaka mahali pa juu na kuteketeza uvumba kwa miungu yake - asema Yahwe. 36 Hivyo moyo wangu unamwombolezea Moabu kama zomari. Moyo wangu unaomboleza kama zomari kwa ajili ya watu wa Kir Heresi. Utajiri walioupata umekwisha. 37 Maana kila kichwa kina upaa na kila kidevu kimenyolewa. Chale zipo katika kila mkono, na nguo za magunia katika viuno vyao. 38 Maombolezo yapo kila mahali, juu ya kila paa la nyumba ya Moabu na katika masoko ya Moabu. Kwa maana nimeivunja Moabu kama chungu kisichotakiwa tena - asema Yahwe. 39 Jinsi gani imeharibiwa! Jinsi wanavyopiga kelele katika maombolezo yao! Moabu ameigeuza kwa aibu! Hivyo Moabu atakuwa kitu cha kuchekwa na kitisho kwa wote wanaomzunguka.” 40 Maana Yahwe asema hivi, “Tazama, adui atakuja akiruka kama tai, akieneza mabawa yake juu ya Moabu. 41 Keriothi umetekwa, na ngome zake zimekamatwa. Maana siku hiyo myoyo ya askari wa Moabu itakuwa kama mioyo ya wanawake katika uchungu wa kujifungua. 42 Hivyo Moabu utaharibiwa kama watu, kwa kuwa walijivuna kinyume changu, Yahwe. 43 Hofu na shimo, na mtego vinakujia, watu wa Moabu - asema Yahwe. 44 Kila akimbiaye kwa sababu ya hofu ataanguka shimoni, na kila atokaye shimoni atanaswa na mtego, maana nitayaleta haya juu yao katika mwaka wa kisasi changu dhidi yao - asema Yahwe. 45 Wakimbiao watasimama katika kivuli cha Heshboni bila nguvu, maana moto utatoka Heshboni, miale kutoka katikati ya Sihoni. Utateketeza paji la uso wa Moabu na juu ya vichwa vya watu wenye majivuno. 46 Ole wako, Moabu! watu wa Kemoshi wameangamizwa, Kwa maana wana wako wamechukuliwa kama mateka na binti zako matekani. 47 Lakini nitazirejesha siku njema za Moabu katika siku zijazo - asema Yahwe.” Hukumu ya Moabu inaishia hapa.

< Yeremia 48 >