< Zaburi 3 >

1 Zaburi ya Daudi. Alipomkimbia mwanawe Absalomu. Ee Bwana, tazama adui zangu walivyo wengi! Ni wengi kiasi gani wanaoinuka dhidi yangu! 2 Wengi wanasema juu yangu, “Mungu hatamwokoa.” 3 Lakini wewe, Ee Bwana, ni ngao pande zote; umeniwekea utukufu na kuinua kichwa changu. 4 Ninamlilia Bwana kwa sauti kuu, naye ananijibu kutoka mlima wake mtakatifu. 5 Ninajilaza na kupata usingizi; naamka tena, kwa maana Bwana hunitegemeza. 6 Sitaogopa makumi elfu ya adui, wanaojipanga dhidi yangu kila upande. 7 Ee Bwana, amka! Niokoe, Ee Mungu wangu! Wapige adui zangu wote kwenye taya, vunja meno ya waovu. 8 Kwa maana wokovu watoka kwa Bwana. Baraka yako na iwe juu ya watu wako.

< Zaburi 3 >