< Hesabu 4 >

1 Bwana akawaambia Mose na Aroni, 2 “Wahesabu Wakohathi walio sehemu ya Walawi kwa koo zao na jamaa zao. 3 Wahesabu wanaume wote wenye umri wa miaka thelathini hadi hamsini wanaokuja kutumika katika kazi ya Hema la Kukutania. 4 “Hii ndiyo kazi ya Wakohathi katika Hema la Kukutania: Watatunza vitu vilivyo vitakatifu sana. 5 Wakati kambi inapohamishwa, Aroni na wanawe wataingia ndani na kushusha lile pazia la kuzuilia na kufunika nalo Sanduku la Ushuhuda. 6 Kisha watafunika juu yake na ngozi za pomboo, na kutandaza juu yake kitambaa cha rangi ya buluu iliyokolea na kuingiza mipiko mahali pake. 7 “Juu ya meza ya mikate ya Wonyesho watatandaza kitambaa cha buluu na waweke sahani juu yake, masinia, bakuli na magudulia kwa ajili ya sadaka za kinywaji; mkate ule ambao upo hapa daima utabaki juu yake. 8 Juu ya hivyo vitu watatandaza kitambaa chekundu na kufunika kwa ngozi za pomboo na kuweka mipiko yake mahali pake. 9 “Watachukua kitambaa cha buluu na kufunika kinara cha taa kilicho kwa ajili ya nuru, pamoja na taa zake, mikasi yake, sinia zake, magudulia yake yote yaliyotumika kuwekea mafuta. 10 Kisha watakisokotea pamoja na vifaa vyake vyote katika ngozi za pomboo na kukiweka kwenye jukwaa lake. 11 “Juu ya madhabahu ya dhahabu watatandaza kitambaa cha buluu na kukifunika kwa ngozi za pomboo na kuweka mipiko yake mahali pake. 12 “Watavichukua vyombo vyote vinavyotumika kuhudumia mahali patakatifu, watavisokotea kwenye kitambaa cha buluu na kufunika kwa ngozi za pomboo, na kuviweka juu ya miti ya kuchukulia. 13 “Wataondoa majivu kutoka madhabahu ya shaba na kutandaza kitambaa cha zambarau juu yake. 14 Kisha wataweka vyombo vyote juu yake vinavyotumika kwa kuhudumia madhabahuni pamoja na vyombo vya kutolea moto, nyuma, miiko na mabakuli ya kunyunyizia. Juu yake watatandaza ngozi za pomboo ya kufunika, na kuweka mipiko mahali pake. 15 “Baada ya Aroni na wanawe kumaliza kazi ya kufunika samani takatifu na vyombo vyake vyote, watu watakapokuwa tayari kungʼoa kambi, Wakohathi watakuja kufanya kazi ya kubeba. Lakini wasije wakagusa vitu vitakatifu la sivyo watakufa. Wakohathi ndio watakaobeba vile vitu vilivyomo katika Hema la Kukutania. 16 “Eleazari mwana wa Aroni, kuhani, ndiye atakayesimamia mafuta kwa ajili ya taa, uvumba wenye harufu nzuri, sadaka za kila siku za nafaka na mafuta ya upako. Ndiye atakayekuwa msimamizi wa maskani yote ya Bwana na kila kitu kilichomo ndani mwake pamoja na samani takatifu na vyombo vyake.” 17 Bwana akawaambia Mose na Aroni, 18 “Hakikisheni kwamba koo za kabila la Wakohathi hawatengwi kutoka Walawi. 19 Ili wapate kuishi wala wasife wanapokaribia vitu vitakatifu sana, uwafanyie hivi: Aroni na wanawe watakwenda mahali patakatifu na kumgawia kila mtu kazi yake, na kwamba ni nini atakachochukua. 20 Lakini Wakohathi hawaruhusiwi kuingia ndani ili kuangalia vitu vitakatifu, hata kwa kitambo kidogo, la sivyo watakufa.” 21 Bwana akamwambia Mose, 22 “Wahesabu pia Wagershoni kwa jamaa zao na koo zao. 23 Wahesabu wanaume wote wenye umri wa miaka thelathini hadi hamsini ambao huja kutumika katika Hema la Kukutania. 24 “Hii ndiyo huduma ya koo za Wagershoni wakati wanapofanya kazi na kubeba mizigo. 25 Watabeba mapazia ya maskani. Hema la Kukutania, kifuniko chake na kifuniko cha nje cha ngozi za pomboo, mapazia ya maingilio ya Hema la Kukutania, 26 mapazia ya ua unaozunguka Maskani na madhabahu, pazia la maingilio, kamba na vifaa vyote vinavyotumika katika huduma yake. Wagershoni watafanya yote yatakiwayo kufanyika na vitu hivi. 27 Utumishi wao wote ukiwa ni kuchukua au wa kufanya kazi nyingine, utafanyika chini ya maelekezo ya Aroni na wanawe. Mtawapangia kama wajibu wao yote watakayoyafanya. 28 Hii ndiyo huduma ya koo za Wagershoni katika Hema la Kukutania. Wajibu wao utakuwa chini ya maelekezo ya Ithamari mwana wa kuhani Aroni. 29 “Wahesabu Wamerari kwa koo zao na jamaa zao. 30 Wahesabu wanaume wote kuanzia umri wa miaka thelathini hadi hamsini ambao watakuja kutumika katika Hema la Kukutania. 31 Huu ndio wajibu wao wanapofanya huduma katika Hema la Kukutania: kubeba miimo ya Maskani, mataruma yake, nguzo na vitako, 32 nguzo za ua unaozunguka pamoja na vitako vyake, vigingi vya hema, kamba, vifaa vyake vyote na kila kitu kinachohusiana na matumizi yake. Kila mtu mpangie vitu maalum vya kubeba. 33 Huu ndio utumishi wa koo za Merari kama watakavyofanya kazi katika Hema la Kukutania, chini ya maelekezo ya Ithamari mwana wa kuhani, Aroni.” 34 Mose, Aroni na viongozi wa jumuiya wakawahesabu Wakohathi kwa koo zao na jamaa zao. 35 Wanaume wote kuanzia umri wa miaka thelathini hadi hamsini ambao walikuja kutumika katika Hema la Kukutania, 36 waliohesabiwa kwa koo zao, walikuwa 2,750. 37 Hii ilikuwa ndiyo jumla ya wote wale wa koo za Wakohathi ambao walitumika katika Hema la Kukutania. Mose na Aroni waliwahesabu kufuatana na amri ya Bwana kupitia kwa Mose. 38 Wagershoni walihesabiwa kwa koo zao na jamaa zao. 39 Watu wote kuanzia umri wa miaka thelathini hadi hamsini ambao walikuja kutumika katika Hema la Kukutania, 40 waliohesabiwa kwa koo zao na jamaa zao, walikuwa 2,630. 41 Hii ilikuwa ndiyo jumla ya wale wa koo za Gershoni ambao walitumika katika Hema la Kukutania. Mose na Aroni waliwahesabu kufuatana na amri ya Bwana. 42 Wamerari walihesabiwa kwa koo zao na jamaa zao. 43 Wanaume wote kuanzia umri wa miaka thelathini hadi miaka hamsini ambao walikuja kutumika katika Hema la Kukutania, 44 waliohesabiwa kwa koo zao, walikuwa 3,200. 45 Hii ilikuwa ndiyo jumla ya wale wa koo za Wamerari. Mose na Aroni waliwahesabu kufuatia amri ya Bwana kupitia kwa Mose. 46 Hivyo Mose, Aroni na viongozi wa Israeli waliwahesabu Walawi wote kwa koo zao na jamaa zao. 47 Wanaume wote wenye umri kuanzia miaka thelathini hadi hamsini waliokuja kufanya kazi ya kuhudumu na kubeba Hema la Kukutania 48 walikuwa watu 8,580. 49 Kwa amri ya Bwana kupitia Mose, kila mmoja aligawiwa kazi yake na kuambiwa kitu cha kubeba. Hivyo ndivyo walivyohesabiwa kama Bwana alivyomwamuru Mose.

< Hesabu 4 >